Breaking News
recent

UONGOZI WA MKOA WA IRINGA WAAGIZWA KUWATAFUTIA MAKAZI YA KUDUMU WAATHIRIKA WA MAFURIKO PAWAGA

Waziri wa nchi ofisi ya rais tawala za mikoa na serikali za mitaa Tamisemi George Simbachawene ameuagiza uongozi wa mkoa wa Iringa kuwatafutia maeneo ya makazi ya kudumu waathirika wa mafuriko.

Waathirika hao wanaendelea kuokolewa kwenye mafuriko katika mashamba ya mpunga Pawaga ili kuhakikisha hakuna mtu anayerudi kuweka makazi ya kudumu katika maeneo hayo ili eneo hilo libakie la mashamba pekee.

Waziri Simbachawene amesema hayo alipowatembelea waathirika wa mafuriko waliookolewa kutoka kwenye mashamba ya mpunga Pawaga walikokuwa wamezungukwa na maji na kusema kuwa kuanzia sasa serikali inapiga marufuku vibanda vya muda pamoja na nyumba za kudumu kwenye mashamba hayo ili kuepusha kujirudia kwa janga hilo.
               Waziri wa nchi ofisi ya rais tawala za mikoa na serikali za mitaa Tamisemi George Simbachawene
Akitoa taarifa ya zoezi la uokoaji kaimu mkurugenzi wa halmashauri ya Iringa Bibi Lucy Nyalu amesema mpaka sasa watu walio kwenye kambi za muda wamefikia 419 ambapo idadi hiyo imepungua kutokana na baadhi yao kuchukuliwa na ndugu zao ama kuondoka makwao.

Waziri Simbachawene ameupongeza uongozi wa mkoa wa Iringa kwa juhudi za uokoaji zinazoendelea hadi sasa kukiwa hakuna kifo hata kimoja kilichokwisharipotiwa licha ya changamoto za ukosefu wa vifaa vya uokoaji na kuwaomba wadau mbalimbali kushirikiana na serikali kusaidia waathirika hao kwa hali na mali ambapo mkuu wa mkoa wa Iringa Bibi Amina Masenza amewataka waathirika hao kudumisha usafi ili kujiepusha na maambukizi ya ugonjwa wa kipindupindu.


Mapema kabla ya ziara ya waziri George Simbachawene shirika la afya duniani WHO limekabidhi vifaa mbalimbali ikiwemo dawa za kusafisha maji zenye thamani ya shilingi milioni 25 kwa lengo la kusaidia kuzuia mlipuko wa ugonjwa wa kipindupindu kwenye kambi hizo za waathirika wa mafuriko huku waziri Simbachawene akikabidhi shilingi mil.5 zilizochangwa na watumishi wa ofisi yake..
gmbongo tha entertainer

gmbongo tha entertainer

No comments:

Post a Comment

Powered by Blogger.